Sunday 15 June 2014

TFF YASIMAMISHA UCHAGUZI SIMBA

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limetangaza kusimamisha uchaguzi wa Simba uliopangwa kufanyika Juni 29.


Rais wa TFF, Jamal Malinzi amewaambia waandishi wa habari hivi punde kwamba wamesimamisha uchaguzi huo na kuiagiza Simba kuunda kamati ya maadili.

Baada ya hapo, rufaa zilizokatwa na wanachama wakiwapinga baadhi ya wagombea zitapelekwa kwenye Makati hiyo.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari leo kwenye makao makuu ya TFF katikati ya jijini la Dar es Salaam, Malinzi alisema TFF wameona huenda utaratibu unavyokwenda unaweza kuathiri uchaguzi huo.

"Hivyo TFF inawaagiza Simba kuunda kamati ya maadili ambayo itachukua uamuzi wa kuyashughulikia malalamiko ya wanachama baada ya mchakato wa kamati ya uchaguzi.
"Lakini ikitokea kuna watu hawajaridhishwa na hilo, basi moja kwa moja watakata rufaa kwenye kamati ya maadili ya TFF," alisema huku akitaja kutumia katiba ya Simba ibara ya 16 kifungu 1(e) na ibara ya 30 kifungu (h).

Baada ya kamati ya uchaguzi ya Simba kukamilisha michakato yote, rufaa ziliwasilishwa kwenye kamati ya rufaa ya TFF ambayo ilitoa uamuzi wa kumrudisha mgombea wa Urais Michael Wambura.

Lakini wanachama wengine wakakata rufaa wakianisha mambo kadhaa likiwemo suala la Wambura kugushi barua ya katibu mkuu wa zamani wa Simba, Evodius Mtawala kama ambavyo Mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Simba, Dokta Damas Daniel Ndumbaro alivyosema.

Kutokana na hali hiyo, suala limeonekana kuwa gumu na TFF inalirudisha suala hilo Simba kwa maana moja au nyingine.

No comments:

Post a Comment