Thursday 26 June 2014

YANGA YATEMA NYOTA 11

WACHEZAJI 11 waliochezea Yanga msimu uliopita wameondolewa kwenye kikosi cha timu hiyo siku moja kabla ya ujio wa Mbrazil Marcio Maximo.
Yanga inatarajia kumtangaza rasmi Maximo anayetua nchini leo Jumanne kuwa Kocha mkuu wa timu hiyo lakini kabla hilo halijafanyika wachezaji hao 11 wametupiwa virago vyao kutokana na kutokidhi matakwa ya mahitaji ya bosi huyo mpya.
Wachezaji walioachwa ni pamoja na Athumani Iddi ‘Chuji’ na David Luhende ambao walikuwa na namba kwenye kikosi cha kwanza msimu uliopita. Chuji aliingia kwenye mgogoro na klabu hiyo mwezi Desemba mwaka jana baada ya kuonyesha utovu wa nidhamu kwenye mechi ya Nani Mtani Jembe Yanga ilipochapwa mabao 3-1 na Simba.
Luhende ameenguliwa kutokana na kugoma kuongeza mkataba mapema mwaka huu walipopatiwa mikataba ya pamoja na wachezaji wengine wa klabu hiyo kwa madai kuwa mikataba hiyo haikuambatana na marekebisho ya maslahi yao pamoja na fedha za usajili.
Wachezaji wengine walioachwa ni Hamis Thabit, Yusuph Abdul, Reliants Lusajo, Shaban Kondo na Ibrahim Job wakati makinda Bakari Masoud, Rehani Kibingu, George Banda na Abdallah Mguhi ‘Messi’ waliokuwa kwenye timu ya vijana chini ya miaka 20 nao wakiachwa.
Taarifa rasmi iliyotolewa na Yanga jana Jumatatu ilieleza kuwa majina hayo ni orodha ya awali ya wachezaji watakaoachwa kabla ya kuanza kwa msimu mpya,viongozi wa usajili tayari wameshaanza kutafuta wachezaji wa kuziba nafasi hizo. Wachezaji wengine walio kwenye hatihati ya kuachwa ni pamoja na Said Bahanuzi, Jerry Tegete na kipa Juma Kaseja.
Maximo aliiambia Mwanaspoti nchini Brazil kwamba anatua nchini kuisuka Yanga imara na akasisitiza anataka iwe mfano Afrika. GAZETI LA MWANASPOTI

No comments:

Post a Comment