Tuesday 10 June 2014

Friends of Simba waidhibiti Yanga

KAMA Yanga ilikuwa na ndoto ya kupata saini ya straika namba moja wa Simba, Amissi Tambwe wameumia. Friends of Simba wamesoma mchezo wakaamua kuingia msituni wenyewe.
Kundi hilo lenye wanachama wenye ushawishi mkubwa kwenye mambo mbalimbali, wanajua kwamba baadhi ya vigogo wa Yanga wamewahi kufanya mazungumzo na Tambwe kwa siri kubwa wakimshawishi asitishe mkataba wake na Simba.
Tambwe alitoa masharti matatu ya kutekelezwa ili arudi Simba msimu ujao ikiwemo kuongezewa mshahara na kuboreshwa kwa vipengele vya mkataba wake na kulipwa malimbikizo yake ya usajili.
Akizungumza na Mwanaspoti Evans Aveva mmoja wa vigogo wa Friends alisema wameshaweka mambo yote ya Tambwe sawa imebaki utekelezaji tu ambao utafanyika baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa Simba.
Aveva ambaye anagombea nafasi ya Urais katika uchaguzi ujao wa Simba ameliambia Mwanaspoti kuwa kila kitu kipo sawa na tangu alipochukua fomu kugombea amepokea simu nyingi za mashabiki ambao moja ya kazi waliyomtaka kuifanya ni kuhakikisha Tambwe haendi Yanga.
“Unajua tuna uzoefu mkubwa wa mambo ya usajili katika klabu hii, katika mwaka wa kwanza ni vigumu kumpa maslahi makubwa mchezaji ambaye ndiyo kwanza anajiunga na timu lakini anapofanya vizuri kila kitu kinajulikana kwamba kuna haja ya kuongeza vitu vichache katika kumpa nguvu,”alisema Aveva.
“Tayari tumeshajadili hilo kwa pamoja kila kitu kitafanyika kwa umakini, atulie maisha mazuri yanakuja tusubiri uchaguzi umalizike,”alisisitiza. Friends of Simba wamemsimamisha Aveva kwenye nafasi ya Urais na wamekuwa wakimpa sapoti kubwa ingawa kwenye nafasi ya Makamu wa Rais wanaonekana kugawanyika.
SOURCE:Mwanaspoti

No comments:

Post a Comment