Wednesday 29 April 2015

Tanzania yaomba uenyeji CAF U17

TFF kwa kushirikiana na serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo imeomba kuwa mwenyeji wa michuano ya Afrika chini ya umri wa miaka 17 (U17) kwa mwaka 2019
TFF kwa kushirikiana na serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo imeomba kuwa mwenyeji wa michuano ya Afrika chini ya umri wa miaka 17 (U17) Goal inafahamu
RAIS wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) Jamal Malinzi alithibitisha hilo alipokua akifungua semina ya makocha wakufunzi inayoanza leo Aprili 27 na kumalizika Mei 2 2015, ufunguzi huo umefanyika kwenye ofisi za TFF zilizopo Ilala jijini Dar es Salaam.
Goal ilikuwepo wakati wa ufunguzi huo na Rais Malinzi amezungumzia mipango ya muda mrefu ya TFF katika kuhakikisha soka la Tanzania linasonga mbele na kuendana na ushindani uliopo toka kwenye nchi ambazo tayari zimepiga hatua kwenye soka la Afrika na Dunia kwa ujumla.

“Kwanza tutaanza na maandalizi kwa ajili ya kufuzu kushiriki michuano ya kombe la Dunia na ile ya mataifaya Afrika. Tumepanga kuweka kambi yetu Ethiopia kwa ajili ya maandalizi ya mchezo dhidi ya Misri utakaochezwa mwezi Juni mwaka huu”, amesema Malinzi.
“Pia kwa sasa tunaiandaa timu ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 (U17) kwa ajili ya mashindano ya Afrika yatakayochezwa mwaka 2017. Timu hiyo imeanza kuandaliwa chini ya mwalimu Adolf Rishard kwa kuwachukua vijana waliofanya vizuri mwaka huu kwenye michuano ya Copa-CocaCola wengi wao wakiwa chini ya umri wa miaka 15”, Malinzi amesema.
“Lakini katika kuhakikisha tunafanya vizuri kwenye soka, tumeanzisha mashindano ya vijana wenye umri chini ya miaka 13 yatakayofanyika Mwanza mwezi Juni ikiwa ni kuwekeza kwenye soka la vijana. Vijana ambao watafanya vizuri watabakizwa kwenye kituo cha Alliance na baadae watajumuishwa kwenye kikosi cha timu ya U17 na timu ya Taifa”, Malinzi aliongeza.
Malinzi amesema TFF kwa kushirikiana na serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo imeomba kuwa mwenyeji wa michuano ya Afrika chini ya umri wa miaka 17 (U17) kwa mwaka 2019 na tayari barua ya kuomba kuwa mwenyeji imeshalifikia shirikisho la mpira wa miguu Afrika (CAF).
Mwisho wa ufunguzi wake akawaomba washiriki wa mafunzo hayo kuyatumia vyema mafunzo watakayoyapata kwa kuendeleza mchezo wa soka sehemu watokazo lakini na taifa kwa ujumla wakisaidiana na waalimu wa timu za Taifa.
Rais wa zamani wa TFF Leodegar Tenga, lakini kwa sasa ni mjumbe wa CAF ambaye ni mmoja wa washiriki wa semina hiyo, ameishauri TFF kuwekeza kwenye soka la vijana ambao watadumu kwa muda mrefu kwenye timu ya taifa.
“Nchi nyingi zilizopata mafanikio kwenye soka zimewekeza kwa vijana kwa muda mrefu, hivyo hata sisi kama tunahitaji kufikia hatua ya kucheza kombe la dunia na michuano ya Afrika ni lazima tuanzie kwa vijana”, amesema Tenga.
Kama kungekuwa na makombe ya dunia mawili basi sisi tungeomba tupangwe na nchi tunazozimudu, lakini kombe ni moja na tunatakiwa tupambane na hao tunaoona wametuzidi uwezo. Lakini tukiweka mipango ya muda mrefu kwa vijana tutafanikiwa”, alimaliza Tenga.
Sunday Kayuni ndiye mkufunzi mkuu wa semina hiyo lakini atasaidiwa na kocha wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ Mart Nooij ambaye amealikwa kwenye semina hiyo.

No comments:

Post a Comment