Monday 13 April 2015

Match Report: Mtibwa 1- 1 Azam, Hali tete kwa Mabingwa

HALI bado ni mbaya kwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara Azam FC baada ya jioni ya leo kulazimishwa sare ya 1-1 na Mtibwa Sugar
HALI bado ni mbaya kwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara Azam FC baada ya jioni ya leo kulazimishwa sare ya 1-1 na Mtibwa Sugar katika mchezo uliopigwa kwenye dimba la Manungu Turiani Morogoro.
Matokeo hayo yanaifanya Azam kupoteza kabisa matumaini ya kutetea ubingwa wake msimu huu kwa kufikisha pointi 38 huku vinara wanaoongoza ligi hiyo Yanga wakiwa na pointi 43 na kesho wanashuka tena uwanja wa taifa Dar es Salaam kucheza na Mbeya City.
Katika mchezo wa leo Azam ndio walikuwa wa kwanza kuandika bao dakika ya 17 kupitia kwa nahodha msaidizi Himid Mao ‘Ninja’, lakini dakika tatu baadaye Musa Hassan Mgosi aliisawazishia Mtibwa Sugar.
Vijana wa kocha George Nsimbe ‘Best’ walijitahidi kupigana kwa ajili ya kupata ushindi ili angalau kuikaribia Yanga ambayo kabla ya mchezo huo ilikuwa mbele kwa mchezo mmoja lakini Mtibwa Sugar walikataa kabisa kuendeleza rekodi mbaya ya kufungwa na Azam nyumbani.
Mshambuliaji Didier Kavumbagu alipata nafasi nzuri dakika ya 68 lakini aliweza kupiga nje huku Musa Mgosi naye akashindwa kuwa na maelewana mazuri na mshambuliaji mwenzake Amme Ali na hadi mwisho matokeo kubaki sare.

Kwa matokeo hayo Mtibwa Sugar waliopo nafasi ya 12 wamefikisha pointi 24 lakini bado wanatakiwa kupambana ili kuepouka kushuka daraja kutokana na matokeo mabaya wanayoendelea kuyapata na sasa imebakiwa na michezo mitano kabla ya msimu kumalizika.
Leo kabla ya mchezo huo uongozi wa Mtibwa Sugar ulimrudisha kundini aliyekuwa kocha wa timu hiyo siku za nyuma Salum Mayanga ambaye kwa sasa ni kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kwa ajili ya kumsaidia kocha wa sasa Mecky Maxime kumshauri mambo ya kiufundi ili kuinusuru timu hiyo.
Kutokana na mazingira hayo ilitarajiwa mechi ya leo ingekuwa ni ya ushindani na yenye kashikashi nyingi, lakini katika dakika zote 90 timu zilicheza mpira wa kawaida.
Baada ya mechi ya leo, Azam wanakwenda Tanga kucheza mechi ya kiporo Jumatano ya wiki ijayo wakati Mtibwa Sugar wao wanasafiri kwenda Mbeya kuwavaa vibonde wa ligi kuu, timu ya Tanzania Prisons Jumapili ya wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment