Tuesday 17 March 2015

Match Preview: Mgambo JKT – Simba, Msimbazi kuendeleza ubabe

Simba inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu nzuri ya kushinda mechi tatu mfululizo
KIKOSI cha wekundu wa msimbazi Simba kesho kinatarajia kushuka kwenye uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga kupambana na wenyeji Mgambo JKT ukiwa ni mwendelezo wa mechi za ligi ya Vodacom Tanzania bara.
Simba inayonolewa na kocha Mserbia Goran Kopunovic, inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na kumbukumbu nzuri ya kushinda mechi tatu mfululizo kwa kuzifunga Tanzania Prisons,Yanga na Mtibwa Sugar.
Mbali ya Simba kuingia kwenye mchezo huo na rekodi nzuri lakini pia inajivunia kiwango bora na mabao ya kuvutia kutoka kwa mshambuliaji wao wa kimataifa kutoka nchini Uganda Emmanuel Okwi.
Simba inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ya Vodacom ikiwa na pointi 29 na michezo 18 siku za karibuni imeonyesha kiwango cha kuvutia na kufufa matumaini kwa mashabiki wa timu hiyo kwamba huenda wakatwaa ubingwa au kumaliza nafasi ya pili msimu huu.

Lakini pamoja na kiwango bora walichokuwa nacho Simba kwa sasa wanapaswa kucheza kwa tahadhari katika mchezo wa leo kwani Mgambo JKT siyo timu ya kubeza hasa inapokuwa nyumbani na Simba haijawahi kupata ushindi kwenye uwanja wa Mkwakwani katika misimu mitatu iliyopita.
Mgambo inashika nafasi ya 10 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 21 na katika mechi iliyopita iliweza kuifunga Ndanda FC mabao 3-1 kwenye uwanja huo hivyo Simba isitarajie kupata mteremko.
Kocha Bakari Shime, wa Mgambo JKT, amesema amekiandaa kikosi chake kwa ajili ya kuikabili Simba na anauhakika wataendeleza wimbi la ushindi kama walivyofanya kwa Ndanda FC Machi 8.
“Najua Simba ni timu nzuri na kwa sasa wapo kwenye kiwango bora lakini hatuwezi kukubali kufungwa nyumbani ligi inakwenda mwishoni na sisi tupo kwenye nafasi mbaya tunalazimika kushinda ili kujiepusha na janga la kushuka daraja,”amesema Shime.
Kocha Shime ameiambia Goal ataendelea kukitumia kikosi chake kile kilichoanza kwenye mchezo uliopita akiamini kuwa anaweza kupata matokeo dhidi ya Simba ambayo kwa sasa inaonekana kuimarika zaidi baada ya kushinda mechi zake tatu zilizo pita.
Kwaupande wake kocha Goran Kopunovic wa Simba ameonyesha wasiwasi wake na hali mbaya ya uwanja wa Mkwakwani lakini akaahidi kuzungumza na wachezaji wake ili waweze kupambana na kupata pointi tatu ili kuendelea kuzifukuzia timu za Azam na Yanga zilizopo kileleni.
“Uwanja huu ni mbovu mara ya mwisho tulicheza na Coastal Union na mambo hayakwenda vizuri lakini hatuna namna lazima tucheze nimezungumza na wachezaji wangu wote kuhakikisha tunapambana kwa dakika zote 90 ili kupata ushindi,”amesema Kopunovic.
Mgambo JKT huwa na utaratibu wa kukaza kwa kuhakikisha haipotezi mechi za mzunguko wa pili, hasa zinazochezwa Uwanja wa nyumbani, Mkwakwani.
Haijawahi kufungwa na Yanga wala Simba kwenye Uwanja wa Mkwakwani tangu ipande ligi kuu msimu miwili iliyopita na msimu uliopita ilizifunga timu zote mbili kubwa za Simba na Yanga ilianza na Simba ikashinda 1-0 na baada ya hapo ikaifunga Yanga 2-1 kwenye uwanja huo.

No comments:

Post a Comment